Jumatatu, 24 Juni 2013

BAJETI YA TRILIONI 18.2 LEO

BUNGE linatarajiwa kupitisha Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014 ya Sh trilioni 18.2, baada ya wabunge kumaliza kuijadili wiki iliyopita. Katika fedha hizo, zaidi ya Sh trilioni 10 ni za matumizi ya kawaida na zaidi ya Sh trilioni tano ni kwa ajili ya matumizi ya maendeleo. Kabla ya kuahirisha kikao cha Bunge baada ya kipindi cha maswali na majibu Ijumaa wiki iliyopita, Spika wa Bunge, Anne Makinda, alisema kwa mujibu wa Kanuni za Bunge, Bajeti ya Serikali inatakiwa kujadiliwa kwa siku zisizozidi saba.

“Bajeti hii imejadiliwa kwa siku nne na wabunge walioomba kuijadili wamefanya hivyo, sasa naufunga mjadala,” alisema Spika wiki iliyopita wakati akihitimisha mjadala huo.

Spika Makinda alisema bajeti hiyo itapitishwa na wabunge ambao wataitwa majina mmoja mmoja na kila mmoja kutamka ndio au hapana, kwa mujibu wa Ibara 107 (2) ya Kanuni za Bunge.

Sehemu hiyo inasema: “Uamuzi wa Bunge wa kupitisha au kutopitisha Bajeti ya Serikali utafanywa kwa kupiga kura ya wazi kwa kuita jina la mbunge mmoja mmoja.”

Spika Makinda pia aliwakumbusha wabunge kuwa Rais Jakaya Kikwete anaweza kulivunja Bunge iwapo litakataa kupitisha Bajeti ya Serikali.

Mjadala huo wa Bajeti ya Serikali ulifanyika kwa siku nne bila kuhusisha wabunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambao ndiyo wanaunda Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni.

Wabunge hao walikuwa Arusha wakati wote wa mjadala wa bajeti ya serikali wakihudhuria mazishi ya watu waliokufa katika mlipuko wa bomu uliotokea wiki iliyopita katika mkutano wa uchaguzi mdogo wa udiwani huko Kata ya Soweto mkoani Arusha.

Wakati huo huo, wabunge wa CCM jana waliketi kama Kamati ya Chama ndani ya Bunge (Party Cuaucus), kuweka mikakati ya kuipitisha bajeti hiyo.

Habari zilizopatikana zilisema kikao hicho kilikuwa ni cha ‘kuwekana sawa’ kwa ajili ya kupitisha bajeti ya serikali ya mwaka ujao wa fedha leo, ambayo imepata kutoka kwa wabunge mbalimbali wakiwamo wa chama hicho.

Wakati wa kujadili bajeti hiyo wabunge walitoa ushauri mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutopandishwa ushuru wa petroli na dizeli waliodai kuwa utasababisha kupanda kwa hali ya maisha na badala yake walishauri vitafutwe vyanzo vingine vya mapato.

Waliitaka Serikali kuacha kung’ang’ania ushuru unaotokana na bia, mafuta na sigara kila mwaka.

Mambo mengine yaliyoshauriwa na wabunge waliochangia mjadala huo ni kufuta au kupunguza kwa kiasi kikubwa misamaha ya kodi, haja ya serikali kupunguza matumizi, kuboresha utendaji katika Bandari ya Dar es Salaam, kufufua kwa ukamilifu reli ya kati, kufufua miradi ya kilimo cha umwagiliaji maji na kuboresha kilimo, mifugo na uvuvi hasa wa bahari kuu.

0 comments:

Chapisha Maoni

Call Us Now:

+255 655 732121, +255 716 758595 / +255 762 758595